Wakulima wa Pamba Wafundishwa kutengeneza Mbolea hai waongeze Uzalishaji.

Wakulima wa Pamba kijiji cha Mwambiti kata ya Mwamishali wilayani Meatu Mkoani Simiyu wakitengeeza mbolea hai kwa ajili ya kunyunyizia mashamba ya pamba.

 

.


Na COSTANTINE MATHIAS, Meatu-Simiyu.

 
WAKULIMA wa Pamba kutoka Kijiji cha Mwambiti kata ya Mwamishali wilayani Meatu Mkoani Simiyu wameanza kunufaika na Elimu ya Mbolea hai wanayotengeneza wenyewe kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa zao la Pamba.

 
Mbolea hiyo ambayo inatengenezwa kutoka na malighafi za Asili zinazotokana na masalia ya viumbe hai ikiwemo Majibu, kinyesi cha ng'ombe ma mkaa na kwamba mbolea hiyo imesheheni virutubisho vitatu ambavyo ni Nitrojeni, Phosiforasi na Potasium.

 
Akizungumza wakati wa Uandaaji wa mbolea hiyo, Afisa Kilimo kupitia Mpango wa Jenga Kesho Bora (BBT) katika Kijiji cha Mwambiti, Salome Mathias amesema malighafi za mbolea hiyo hupatikana karibu na makazi ya wakulima, hivyo ni rahisi kutengeneza na haina gharama.

 
Amesema mbolea hiyo ya Asili haina kemikali tofauti na mbolea za viwandani ambazo huharibu udongo na mazingira kwa ujumla.

 
"Mbolea hii imegundulika na imesaidia kuongeza uzalishaji na tija katika zao la Pamba tofauti na mbolea za madukani...katika majaribio ya msimu uliopita tulitengeneza mapipa 42 na kusambazwa kwa wakulima zaidi ya 300 ambapo ilileta natokea chanya na mimea iliyopuliziwa ilikuwa na vitumba 60 mpaka 100" amesema.


Ameeleza kuwa wakulima waliotumia mbolea hiyo, wamevuna kilo 800, 900 mpaka 1200 kwa ekari moja na kabla ya mbolea hai wakulima walikuwa wanavuna kilo 200, 250 mpaka 300.

 
Amemshukuru Bodi ya Pamba Tanzania kwa kuwaletea mbolea hiyo mapema kabisa na inatumika katika Kilimo cha zao la Pamba hai na Pamba ya kawaida kwa sababu pia inadhibiti wadudu na kurutubisha udongo.

 
Afisa Kilimo kutoka Bodi ya Pamba Tanzania, Edward Nyawile amesema mbolea hai ilianza kufanyiwa majaribio katika msimu wa 2023/2024 katika wilaya za Igunga, Meatu, Bunda, Butiama na Kishapu.


Amesema mbolea hiyo imeonyesha tija kwa Wakulima ambao wamefanyiwa majaribio kwa kuongeza uzalishaji kutoka kilo 200 kwa ekari na baada ya kutumia mbolea hao waliipata kilo 800 mpaka 1000 kwa ekari moja.


"Bodi ya Pamba imeona mbolea hai itasaidia wakulima kuongeza tija na uzalishaji katika zao la Pamba, msimu wa 2024/2025 matumizi ya mbolea hai yamelengwa katika wilaya ya Meatu kutoka na kuwa kinara wa uzalishaji wa Pamba hai" amesema.

 
Amesema wanatarajia kutengeneza lita 400,000 za mbolea hai zitakazosambazwa kwa wakulima wa wilaya ya Meatu katika msimu huu na pia kuna wilaya zinaendelea kunufaika na msimu ujao wanatarajia kusambaza lita Mil. 7 za mbolea hai nchi nzima.


Bule Nyolobi, mkulima wa zao la Pamba katika Kijiji cha Mwambiti amesema amepata Mafanikio makubwa ya kuongeza uzalishaji kutokana na kutumia mbolea hai tofauti na awali ambapo alikuwa anapata mavuno haba.

Rhoda Masanja, mkazi na mkulima wa Kijiji cha Mwambiti amesema mbolea hiyo imeongeza mavuno kutoka kuzalisha kilo 300 kwa ekari moja na kufikia kilo 800 mpaka 1000 kwa ekari moja.

 

Mwisho. 



Afisa Kilimo kupitia Mpango wa Jenga Kesho Bora (BBT) katika Kijiji cha Mwambiti, wilaya ya Meatu Mkoani Simiyu, Salome Mathias (wa kwanza kushoto) akielekeza Wakulima wa Pamba wa kijiji hicho namna ya kutengeneza mbolea hai kwa ajili ya kunyunyizia mashamba ya pamba. 




Je, una Tangazo, Picha za Matukio, Taarifa au Habari ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi 0746057557 au 0765402289 au Email : simiyupresstz@gmail.com

0 تعليقات

إرسال تعليق

Post a Comment (0)

أحدث أقدم