RC aagiza maafisa ugani, Simiyu, Mara, Shinyanga kupelekwa TARI Nyakabindi kujifunza.

Msimamizi wa kituo cha usambazaji wa teknologia za kilimo (TARI Nyakabindi) kilichopo viwanja vya Nanenane Wilayani Bariadi Mkoa wa Simiyu Isabera Mrema akitoa maelezo kwa mkuu wa Mkoa wa Mara Kanali Evans Mtambi alitombelea banda la Taasisi ya utafiti wa kilimo nchini (TARI) kwenye maonyesho hayo. (Picha na Derick Milton)



Na Derick Milton, Bariadi.


Mkuu wa Mkoa wa Mara Kanali Evans Mtambi amewaagiza makatibu tawala wa mikoa ya Simiyu, Mara na Shinyanga kuhakikisha kabla ya mwezi Oktoba, 2025 maafisa ugani kwenye halmashauri zao wawe wamefika kwenye kituo cha kuzambaza teknologia za kilimo (TARI NYAKABINDI).


Alisema kuwa maafisa ugani hao wafike kwenye kituo hicho kilichopo Wilayani Bariadi Mkoani Simiyu kwa ajili ya kujifunza teknologia na mbinu za kisasa za kilimo kwa ajili ya kuwasaidia wakulima wazalishe kwa tija.


Mkuu huyo wa Mkoa ametoa maagizo hayo juzi wakati akifunga maonyesho ya Nanenane kanda ya ziwa Mashariki yaliyokuwa yanafanyika kwenye viwanja vya Nyakabindi Wilayani Bariadi Mkoa wa Simiyu.


Alisema kuwa kituo hicho kimekuwa kikitoa mafunzo mbalimbali hadi kwa wakulima na maafisa ugani, ya jinsi ya kuzalisha kwa tija hivyo ni muhimu maafisa hao kupata elimu hiyo.


“ Nitumie nafasi hii kuwaagiza makatibu tawala wa mikoa ya Simiyu, Mara na Shinyanga, kuhakikisha hadi mwezi Oktoba mwaka huu maafisa ugani kwenye halmashauri zenu waje hapa TARI Nyakabindi wajifunze teknologia za kisasa za kilimo,” alisema Kanali Mtambi…


“ Maafisa hao wakipata elimu hiyo wataweza kuitumia kwa wakulima kwenye maeneo yao ya kazi, watawafundisha teknologia hizo za kisasa na wakulima watabadilika na kuanza kwa tija, lakini pia watawasaidia kupata mbegu bora,” aliongeza Kanali Mtambi.


Awali akiwa katika banda la Taasisi ya utafiti wa kilimo chini (TARI) kwenye maonyesho hayo, Mkuu huyo wa Mkoa alipata maelezo kutoka kwa msimamizi wa kituo hicho cha TARI Nyakabindi Isabera Mrema.


Msimamizi huyo wa Kituo alimweleza Mkuu huyo wa Mkoa kuwa kituo hicho kimekuwa kikitoa mafunzo mbalimbali kwa maafisa ugani, wakulima na wadau wengine wa kilimo juu ya teknologia za kisasa.


“ Tunaomba maafisa ugani kwenye hii kanda yetu waje hapa tuwape mafunzo mbalimbali ya teknologia za kisasa, ili waweze kuwasaidia wakulima kuzalisha kwa tija,” alisema Mrema.


MWISHO.



Je, una Tangazo, Picha za Matukio, Taarifa au Habari ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi 0746057557 au 0765402289 au Email : simiyupresstz@gmail.com

0 تعليقات

إرسال تعليق

Post a Comment (0)

أحدث أقدم