MrJazsohanisharma

NMB yakabidhi Mabati 400 kukamilisha madarasa 8 Bariadi.

Meneja Benki ya NMB Kanda ya Magharibi Restus Asenga (wa pili kutoka kushoto) akimkabidhi Bati 400 Mbunge wa Jimbo la Bariadi Mkoani Simiyu Mhandisi Kundo Andrea ( wa pili kutoka kulia) kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa vyumba 8 katika shule za Msingi Mwamijondo na Banemhi zilizoko katika Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi.


Na Derick Milton, Bariadi.


Katika kuhakikisha inaunga mkono juhudi za serikali na wananchi za kuboresha mazingira kwenye sekta ya Elimu nchini Benki ya NMB imetoa mabati 400 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa madarasa katika shule za Msingi Mwamijondo na Banemhi.


Shule hizo zilizoko katika Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi Mkoani Simiyu zimepatiwa mabati hayo yenye thamani ya Sh Milioni 14.4, ambapo katika shule ya Mwamijondo NMB imetoa bati 260 na Banemhi bati 140.


Akikabidhi vifaa hivyo katika hafla iliyofanyika jana kwenye shule ya Msingi Mwamijondo, Meneja wa NMB Kanda ya Magharibi Restus Assenga alisema kuwa mabati hayo yatakamilisha ujenzi wa vyumba 8 kwenye shule zote mbili.


Alisema kuwa mbali na serikali kuendelea kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji kwenye sekta ya elimu, NMB kama mdau umekuwa wajibu wake kuhakikisha inaunga mkono juhudi hizo za serikali.


“ Pamoja na mambo makubwa yote ambayo serikali yetu inaendelea kufanya, sisi kama wadau tunawajibu wa kuunga mkono juhudi hizo za maendeleo kwa kusaidia jamii, kwani wateja wetu pia wapo kwenye hizo jamii,” alisema Assenga.


Alisema kuwa NMB inatambua kuwa elimu ndiyo nguzo kuu ya maendeleo kwa taifa, jambo ambalo limekuwa chachu kwa taasisi hiyo katika kuhakikisha inaunga mkono juhudi za serikali kuboresha sekta hiyo.


Akipokea vifaa hivyo Mbunge wa Jimbo hilo na Naibu Waziri wa Maji Mhandisi Kundo Andrea aliwashukuru NMB kwa vifaa hivyo ambavyo alieleza vitakwenda kukamilisha ujenzi wa madarasa hayo.


Mhandisi Kundo alisema kuwa uwepo wa mazingira mazuri ambayo yamefanywa na serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan yamewezesha taasisi za kifedha nchini kufanya kazi zao na kupata faida ambayo imekuwa neema kwa wananchi.


“ Bila ya mazingira mazuri ya kufanya kazi zao NMB wasingelileta vifaa hivyo, mazingira yamekuwa mazuri ndiyo maana leo tunapokea hivi vifaa ambavyo vitaboresha mazingira ya shule zetu,” alisema Mhandisi Kundo.


MWISHO

Je, una Tangazo, Picha za Matukio, Taarifa au Habari ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi 0746057557 au 0765402289 au Email : simiyupresstz@gmail.com

0 Comments

Post a Comment

Post a Comment (0)

Previous Post Next Post