Rais Samia: Wafanyabiashara tujenge tabia ya kulipa kodi kwa hiari.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan akikata utepe kuashiria kuzinduliwa kwa Ofisi za TRA Mkoa wa Simiyu.


Na Frank Kasamwa.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewahimiza wafanyabiashara kuendeleza utamaduni wa kulipa kodi ili kuiwezesha serikali kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo na kupunguza utegemezi wa mikopo ya nje.


Amesema kuwa masharti ya mikopo kutoka nje yameendelea kuongezeka siku hadi siku, hivyo ni muhimu kwa nchi kuimarisha uwezo wa kukusanya mapato ya ndani ili iweze kujitegemea.


Rais Dkt. Samia alitoa kauli hiyo jana wakati wa uzinduzi wa ofisi za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Simiyu. Amesisitiza kuwa hakuna nchi yoyote duniani inayoweza kujiendesha bila mapato ya kodi.


Ameeleza kuwa ili wananchi waweze kupata huduma bora za kijamii kama maji safi, huduma za afya, umeme na nyinginezo, ni lazima serikali iwe na mapato madhubuti ya ndani, na kila mtu anayestahili kulipa kodi atimize wajibu huo.


"Wananchi wenzangu na wafanyabiashara, wale wanaotukopesha fedha wanaweza kufanya hivyo kwa sababu raia wao wanalipa kodi. Sasa ni mpaka lini tutaendelea kukopa? Hatuhitaji kuendelea kukopa lazima tukusanye kodi zetu wenyewe," alisema Rais Samia.


Katika hatua nyingine, Rais amewataka maafisa wa TRA kukusanya kodi kwa njia rafiki na ya ushirikiano badala ya kutumia nguvu au vitisho.


Amesema kuwa watumishi wa TRA wanapaswa kuzingatia mbinu za kiungwana, kama vile kufanya mazungumzo na wafanyabiashara ambao bado hawajalipa kodi na kukubaliana nao juu ya namna ya kulipa kwa awamu.


"Njia ya kwanza ya kukusanya kodi iwe ni ya kirafiki. Kwa wale ambao hawajalipa, waiteni, fanyeni nao kikao, kubalianeni namna ya kulipa kidogo kidogo ili serikali isipoteze mapato kabisa," alisisitiza.


Rais Samia ameongeza kuwa matumizi ya nguvu katika ukusanyaji wa kodi kama vile kuchukua vifaa vya biashara, nyaraka au kufungia akaunti za benki visiwe chaguo la kwanza, bali litumike pale tu wafanyabiashara wanapokaidi kwa makusudi.


"Matumizi ya nguvu kama kuchukua kompyuta ya mfanyabiashara, vitabu vyake, au kufungia akaunti zake visianze kutumika moja kwa moja. Bali vitumike tu pale mtu anapokaidi makusudi," alisema Rais Dkt. Samia.


Hata hivyo, Rais Samia pia amewataka wafanyakazi wa TRA kufanya kazi kwa weledi na kuhakikisha wanatimiza malengo ya ukusanyaji wa mapato ya serikali.


Amebainisha kuwa serikali imeendelea kuboresha mazingira ya kazi na maslahi ya wafanyakazi wa TRA, ikiwa ni pamoja na kupitisha ajira mpya takribani 1,800 ndani ya mamlaka hiyo.


 

Je, una Tangazo, Picha za Matukio, Taarifa au Habari ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi 0746057557 au 0765402289 au Email : simiyupresstz@gmail.com

0 تعليقات

إرسال تعليق

Post a Comment (0)

أحدث أقدم