MKUU wa Wilaya ya Maswa Aswege Kaminyoge pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama wamesema wameridhishwa na Ujenzi wa miradi ya Maji inayotekelezwa na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (MAUWASA) kwamba inaendana na thamani ya fedha.
Aidha Kaminyoge amesema ameridhika na matumizi ya fedha zinazotolewa na serikali katika miradi ya maji na kwamba fedha za kutekeleza miradi hiyo zimekuwa hazikai kwenye akaunti kwa muda mrefu pindi zinapotolewa na serikali.
Ameyasema hayo juzi wakati akikagua ujenzi wa tenki la kuhifadhia maji lenye ujazo wa lita milioni mbili lilioko kijiji cha Hinduki na ulazaji wa bomba katika tenki la maji lenye ujazo wa lita milioni moja lililoko mjini Maswa.
Alisema serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia imetoa zaidi ya Bil. 2 kwa ajili ya ujenzi wa tenki la maji kwa ajili ya kutoa huduma ya maji kwa wananchi katika mji wa Maswa.
‘’Mradi huu ukikamilika, wananchi wa Mji wa Maswa watapata maji kwa masaa 24 tofauti na ilivyo sasa wanapata maji kwa masaa 8…ninamwaomba Rais Samia na Waziri wa Maji (Jumaa Aweso) waendelee kutoa fedha ili kukamilisha miradi ya maji’’ alisema Kaminyoge.
Alifafanua kuwa mradi huo ukikamilika, wananchi watapa maji kwa uhakika na Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira itapunguza nusu ya gharama za umeme za usambazaji wa maji kutoka milioni 25 kwa mwezi hadi kufikia milioni 10 au 12.
Aliwaonya wananchi kutohujumu miradi ya maji kwa kukata mabomba na endapo watabainika kufanya uhalifu, viongozi wa eneo hilo watachukuliwa hatua za kisheria kwani wanatakiwa kuwa walinzi wa miradi ya maji sababu inawanufaisha wananchi moja kwa moja.
Awali Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Mjini Maswa (MAUWASA) Mhandisi Nandi Mathias alisema wameanza kutekeleza ahadi ya Waziri wa Maji, Jumaa Aweso ya Ujenzi wa tenki la kuhifadhi Maji lita Milioni mbili na ulazaji wa bomba katika tenki la Maji lenye ujazo wa lita Milioni moja.
Mhandisi Nandi Mathias alisema kuwa tayari wameshapokea kiasi cha fedha zaidi ya shilingi Mil. 350 Kwa ajili ya Ujenzi wa tenki hilo ambalo limeshaanza kujengwa katika Kijiji Cha Hinduki.
Mhandisi Nandi alisema pia tayari wameshanunua bomba zenye gharama ya shilingi mil. 250 na kazi ya ulazaji wa bomba katika tenki jipya lililoko kwenye kilima cha Nyalikungu mjini Maswa umeshaanza ambalo Lina uwezo wa kuhifadhi Maji lita Milioni moja.
MWISHO.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira (MAUWASA) Mhandisi Nandi Mathias kipanda ngazi kwa ajili ya kukagua ujenzi wa tenki la kuhifadhia maji lenye ujazo wa lita mil. 2 linalojengwa kijiji cha Hinduki wilayani Maswa.
Ujenzi wa Tenki la Kuhifadhia Maji lenye ujazo wa lita milioni mbili ukiendelea katika kijiji cha Hinduki wilaya Maswa mkoani Simiyu.
إرسال تعليق