Na COSTANTINE MATHIAS, Meatu.
SERIKALI ya Awamu ya sita chini ya Dk. Samia Suluhu Hassan imetoa zaidi ya shilingi mil. 120 ili kuwakomboa wanafunzi wa shule ya msingi Kasela ambao awali walikuwa wakitumia madarasa ya miti.
Wanafunzi hao walikuwa wanatembea umbali wa kilometa 30 kufuata elimu kwenda kijiji cha Lukale wilayani Meatu Mkoani Simiyu.
Afisa Elimu kata ya Bukundi Amani Mohammed amesema shule hiyo ilifunguliwa mwaka 2022 na kwamba ina jumla ya wanafunzi 72 kutoka darasa la kwanza hadi la saba.
Amesema baada ya mwanakijiji mmoja kujenga darasa la miti ili wanafunzi waweze kupata elimu, serikali ilitoa fedha kiasi cha shilingi mil. 120 kupitia Mradi wa UVIKO 19 na kujenga vyumba sita vya madarasa ili kuwanusuru wanafunzi hao.
Ameongeza kuwa baada ya mradi huo kukamilika, serikali pia imetoa kiasi cha shilingi mil. 11 kwa ajili ya ujenzi wa matundu kumi ya vyoo.
Amezitaja changamoto zinazokabili ujenzi wa vyoo vya shule hiyo kuwa ni gharama kubwa za usafirishaji wa vifaa vya ujenzi, upatikanaji mkubwa wa maji ambapo huyafuata umbali wa kilometa 70.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Dk. Yahaya Nawanda amempongeza Mwenyekiti wa CCM Mkoa huo (Shemsa Mohammed) baada ya kutembelea shule hiyo na kuiagiza shule kupeleka fedha za ujenzi wa vyumba vya madarasa.
‘’Ulituagiza tutafute fedha kokote, nasi tukamwomba Rais Samia tukajenga shule hii ya kisasa…samani lilikuwa darasa la watoto la miti na alijitolea mwananchi mmoja kujenga, tunamshukuru Rais Samia kwa kuwajali wananchi wa pembezoni ambao ni wafugaji wa kitaturu, kimasai na wasukuma’’ amesema Dk. Nawanda.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Simiyu Shemsa Mohammed amesema aliitembelea shule hiyo miaka mitatu iliyopita na kukuta hakuna vyumba vya madarasa bali lilikuwa darasa la miti.
‘’Mtu mmoja alijitolea ili watoto wake wasome, tuliongea na DED, DC na Rc bajeti iliyofuata wakapata fedha za Uviko kujenga madarasa…tunamshukuru Rais Samia kwa kujenga madarasa na anaendelea kuhudumia wananchi huku chini’’ amesema.
Amesema wakati anakwenda eneo hilo kusikilia kero, walimweleza kuwa hawajawahi kuona kiongozi yoyote ambapo kwa sasa wanamshukuru Rais Samia kwa kuwaletea maendele huku akiitaka serikali kuwasogezea pia huduma ya zahanati.
MWISHO.
Ujenzi wa vyoo vya shule ya Msingi Kasela wilayani Meatu ukiendelea.
Je, una Tangazo, Picha za Matukio, Taarifa au Habari ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi 0746057557 au 0765402289 au Email : simiyupresstz@gmail.com
Post a Comment