UTPC yazindua Kampeni kupiga vita ukatili wa kijinsia.

 


Muungano wa klabu za waandishi wa habari Tanzania leo umezindua rasmi kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia, ambapo imelenga kuwaunganisha waandishi wa habari nchini pamoja na wadau wengine kupaza sauti kwa pamoja kupinga vita vitendo hivyo.


Kampeni hiyo imezinduliwa leo Mkoani Morogoro, ambapo ilitanguliwa na mafunzo kwa waandishi wa habari zaidi ya 20 kutoka katika mikoa mbalimbali tanzania bara na visiwani yaliyolenga kupiga vita vitendo vya ukatili wa kijinsia.


Akizundua Kampeini hiyo kwa niaba ya Rais wa UTPC Deo Nsokolo, Mjumbe wa Bodi ya UTPC  Lilian Lucas amesema kuwa waandishi wa Habari wanayo nafasi kubwa kupitia kalamu zao kuhakikisha vitendo hya ukatili kwa wanawake na watoto vinakomeshwa.


“ Kwa sasa tuna tatizo kubwa la matukio ya ubakaji na ulawiti wa watoto wa kike na wadogo, kupitia kampeni hii tunaomba wanahabari kuungana kwa pamoja na wadau wengine kuweka nguvu zaidi za kuhakikisha tunakomesha vitendo hivi kwenye jamii,” amesema Lilian.


Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa UTPC Keneth Simbaya amesema kuwa vitendo vya ukatili wa kijisia hasa kwa wanawake na watoto ni miongoni mwa ukiukwaji mkubwa uliokithiri wa haki za binadamu na kuwataka wanahabari kushiriki vyema katika kuielimisha jamii.


Amesema kuwa vyombo vya habari vina nguvu na kubwa sana ya kuifanya jamii kupata mambo ya kujadili, ambapo amewaomba waandishi wa Habari kutumia kampeini hiyo kuifanya jamii ipate cha kujadili kuhusu masuala ya ukatili wa kijinsia na kuyapinga.


"Waandishi wa habari kemeeni vitendo vya ukatili kwa kuandika na kuibua kila aina ya vitendo vinavyosababisha ukatili, na sii hivyo tu badala yake pia iwe sanjari na kutoa elimu kwa kuandaa vipindi pamoja na kuzipa habari zihusuzo ukatili katika vyombo vyetu vya habari". Amesema mkurugenzi.


Naye Afisa Programu, utawala na maendeleo ya Klabu Hilda Kileo amesema Kupitia kampeni hiyo, UTPC itatumia siku16 katika kutoa elimu ikiwemo kuandaa mada na mijadala mbalimbali ikiwemo ndoa na mimba za utotoni, ukeketaji na vitendo vingine kama hivyo ambavyo vimekuwa na madhara makubwa na wakati mwingine hata kugharimu maisha ya watu.


Hilda amesema kuwa Kwa mwaka huu kauli mbiu ya Kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia ni Wekeza, zuia ukatili wa kijinsia.

MWISHO.


Je, una Tangazo, Picha za Matukio, Taarifa au Habari ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi 0746057557 au 0765402289 au Email : simiyupresstz@gmail.com

0 Comments

Post a Comment

Post a Comment (0)

Previous Post Next Post