Afisa Biashara Elimu kwanza, na siyo kukusanya ushuru tu: DC Maswa.

Mkuu wa Wilaya ya Maswa Mkoani Simiyu Aswege Kaminyoge, akizungumza na wajumbe wa Baraza la Biashara la Wilaya hiyo wakati wa uzinduzi wake. 


Na Derick Milton, Maswa.


Mkuu wa Wilaya ya Maswa Mkoani Simiyu Aswege Kaminyoge ameitaka Ofisi ya Biashara katika Halmashauri ya Wilaya hiyo, kazi yao ya kwanza iwe ni kutoa elimu kwa wafanyabiashara ili biashara zao ziweze kukua.


Alisema kuwa kazi ya kwanza ya Afisa Biashara isiwe kukusanya ushuru au kutoa leseni pekee kwa wafanyabiashara, bali iwe kuhakikisha Biashara zinakua mara kwa mara.


Kaminyoge ametoa rai hiyo jana, wakati akizundua Baraza la Biashara la Wilaya hiyo, ambapo ameeleza wafanyabishara wengi bado wanahitaji elimu katika ufanyaji wa biashara zao.


 “ Katika mwongozo wa Mabaraza, unatutaka serikali kuweka mazingira wezeshi kwa wafanyabishara, niwatake maafisa Biashara, kazi yetu ya kwanza iwe Elimu na siyo kukusanya ushuru pekee au kutoa leseni...kazi ya leseni itakuja baadaye,” Alisema Kaminyoge.


Aidha Mkuu huyo wa Wilaya aliwahakikishia wafanyabiashara katika Wilaya hiyo kuwa serikali itaendelea kutatua changamoto zinazowakabili ikiwemo kupunguza utitiri wa kodi ili waweze kufanya shughuli zao kwa amani.


Mratibu wa Mabaraza ya Wilaya na Mikoa kutoka Baraza la Biashara Taifa (TNBC) Marco Chacha akizungumza wakati wa uzinduzi wa Baraza hilo, alisema kuwa lengo la uwepo wa Mabaraza ni kutatua changamoto zinazowakabili wafanyabishara.


Chacha alisema kuwa Baraza la Biashara limeanzishwa kisheria, hivyo linatakiwa kutumika kama jukwaa la kukwamua uchumi katika ngazi mbalimbali na wafanyabiashara kuwasilisha hoja zao kwa serikali.


Mwenyekiti wa Wafanyabiashara katika Wilaya hiyo Winfrida Nige alisema kuwa kilio kikubwa cha wafanyabiashara ndani ya Wilaya hiyo, kilikuwa ni juu ya uanzishwaji wa Baraza hilo ili waweze kuwasilisha changamoto zao.


“ Tunaishukuru sana serikali kwa mara kwanza ndani ya miaka zaidi ya mitatu leo Maswa tunapata Baraza, tunajua hili ndilo jukwaa letu la kutatuliwa changamoto tunazokutana nazo kwenye kazi etu,” alisema Nige.


MWISHO. 

Je, una Tangazo, Picha za Matukio, Taarifa au Habari ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi 0746057557 au 0765402289 au Email : simiyupresstz@gmail.com

0 تعليقات

إرسال تعليق

Post a Comment (0)

أحدث أقدم