Na COSTANTINE MATHIAS, Itilima.
Serikali imetoa kiasi Cha shilingi Bilioni 3.3 kwa ajili ya kujenga Barabara ya kiwango Cha Lami kwa Majaribio, yenye urefu wa kilometa 5.2 katika wilaya ya Itilima Mkoani Simiyu.
Akitoa taarifa ya Ujenzi wa barabara hiyo mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Dkt. Yahaya Nawanda aliyekuwa anakagua barabara, Meneja wa Wakala wa Barabara za mjini na Vijijini (TARURA), wilaya hiyo Mhandisi Reginald Silanga amesema teknolojia hiyo itaokoa gharama za Ujenzi wa barabara kwa asilimia 25.
Mhandisi Reginald amesema wanajenga barabara hiyo ya lami kwa kiwango cha Matabaka ya Udongo yaliyochanganywa na kimiminika Cha Ecozymes Permazyme@ 11x, ambayo ni teknolojia mpya hapa nchini.
Amefafanua kuwa Mradi huo unatekelezwa kati ya TARURA na Kampuni ya M/S Bronze Technology Co. Ltf na utatekelezwa kwa siku 365.
"Teknolojia hii Mbadala ndani ya nchi itaokoa gharama kubwa za Ujenzi wa barabara kwa asilimia 25, gharama ndogo za ukarabati, faida katika mazingira na barabara kutumika kwa muda mrefu" amesema Mhandisi Silanga.
Amefafanua kuwa Mradi huo utajumuisha barabara yenye urefu wa kilometa 5.2, taa za barabarani 40, kalvati 32 na vivuko vya watembea kwa miguu.
Awali Meneja wa TARURA Mkoa wa Simiyu Mhandisi Gaston Gasana ameeleza kuwa Mradi huo ni wa Majaribio na unatekelezwa katika wilaya 11 nchi nzima na kwamba unatekelezwa kwa kutumia njia Mbadala ambayo itapunguza gharama za Ujenzi na barabara hiyo itadumu kwa miaka 10.
Diwani wa Kata ya Lagangabilili, Dotto Chasama amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha hizo ambazo zimelenga kuimarishabna kuboresha barabara.
"Wananchi walikuwa wanapata shida ya barabara, Sasa wamefurahi na wanashukuru baada ya Rais Dkt. Samia kutoa fedha...tunaomba pia kujengewa soko na stendi" amesema Diwani huyo.
Mkuu wa Mkoa huyo Dkt. Yahaya Nawanda amesema Mradi huo wa barabara za lami kwa Teknolojia Mbadala unatekelezwa katika wilaya 11 na Itilima ikiwemo.
Ameioongeza wilaya hiyo kwa kupata bahati ya kujengewa lami kwa Teknolojia Mbadala huku akiwasisitiza wakandarasi kukamilisha kwa wakati pia wasiache madeni kwa mama ntilie baada ya kukamilisha Mradi.
"Lengo la Mradi huu ni kupunguza gharama za Ujenzi, badala ya kutumia fedha nyingi na Rais ametupa kilometa 5, lakini tumeomba tena kilometa 2 ili tukishe kilometa 7...wananchi tutunze Mradi huu na Mkuu wa wilaya utoe elimu kwa wananchi ili watunze miradi hii" amesema Dkt. Nawanda.
Mwisho.
إرسال تعليق