MrJazsohanisharma

WASIRA AWAELEZA WANA-BARIADI CCM ILIVYOANZISHWA.



Na COSTANTINE MATHIAS, Simiyu. 

 

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Steven Wasira amesema kuwa chama hicho kina historia ndefu ya kisiasa hapa nchini hivyo hakiwezi kulinganishwa na vyama vingine kama vile  United Democratic Party (UDP) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

 

 

Amesema kuwa chama hicho kina historia ndefu ya kisiasa hapa nchini kutokana na ukomavu wa kisiasa kwani chama hicho kilianzishwa mwaka 1977 baada ya kuunganishwa kwa vyama vya TANU (Tanganyika African National Union) na ASP (Afro-Shirazi Party) ya Zanzibar.


Ameyasema hayo kwenye Mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Ngulyati, kata ya Ngulyati wilayani Bariadi Mkoani Simiyu kwa lengo la kukagua uhai wa Chama pamoja na kuongea na Wananchi.


“Hiki chama kwa kuwa kilikuwepo muda mrefu kabla ya mfumo wa vyama vingi kurejeshwa mwaka 1992 hivyo kina uzoefu mkubwa katika siasa za Tanzania huwezi kuvilinganisha na vyama kama UDP na Chadema ambavyo bado ni vidogo,”amesema.


Ameongeza kuwa tangu CCM iliporithi mikoba ya TANU na Afro Shiraz imeendelea kusimamia Maendeleo ya watu kwenye sekta za Afya, Elimu, Maji , Umeme, na Barabara.


Wasira amewataka wananchi kuendelea  kuunga mkono chama hicho ambacho kimeendelea kulinda Umoja, amani na mshikamano hapa nchini.


Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Simiyu Shemsa Mohammed amesema kuna Ushirikiano Mkubwa kati ya Chama na serikali hali inayowafanya kutekeleza miradi ya Maendeleo katika Mkoa huo kwa kiwango kizuri.


Mbunge wa Jimbo la Bariadi, Mhandisi Kundo Mathew amesema kwamba Jimbo la Bariadi litaendelea kuwa ngome imara ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutokana na utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.


Mhandisi Kundo amesema wananchi wa Bariadi wanatambua juhudi kubwa zinazofanywa na serikali ya awamu ya sita katika kuboresha huduma za jamii, ikiwemo Elimu, Afya, Miuundombinu, Maji, na Umeme.

 Amebainisha kuwa miradi ya maendeleo imewagusa wananchi wa kila kata, jambo linalothibitisha dhamira ya CCM kuendelea kuwatumikia Watanzania kwa vitendo.

"Leo hii tunashuhudia maendeleo makubwa katika kila sekta hapa Bariadi. Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imeleta miradi mikubwa ya barabara, shule, hospitali, maji safi na salama, na umeme, jambo ambalo limeifanya Bariadi kuwa mfano wa utekelezaji wa Ilani ya CCM kwa vitendo,” amesema Mhandisi Kundo.


Aidha, Mbunge huyo alimhakikishia Makamu Mwenyekiti wa CCM kuwa wananchi wa Bariadi wamejipanga kuhakikisha chama kinapata ushindi mkubwa katika uchaguzi ujao wa Oktoba, akisisitiza kuwa jimbo hilo litaandika historia kwa kupata kura za mafuriko. 


“Tuna imani kubwa na chama chetu na tunatambua kazi nzuri inayofanywa na serikali...hakuna shaka kwamba Bariadi itaendelea kuwa ngome ya CCM na ushindi wetu utakuwa wa kishindo,” ameongeza.


Aidha, ziara hiyo ya Makamu Mwenyekiti wa CCM imeongeza hamasa kwa wanachama na wananchi kwa ujumla, huku viongozi wa chama wakisisitiza umuhimu wa kushiriki kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi ujao. 


Wananchi wa Bariadi wamethibitisha kuwa wataendelea kuwa sehemu ya historia ya ushindi wa CCM kwa kuhakikisha wanajitokeza kwa wingi kupiga kura mwezi Oktoba.


Mwisho.


MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Steven Wasira akiwa kwenye Mkutano wa hadhara Jimbo la Bariadi, uliofanyika katika Kijiji cha Ngulyati wilayani Bariadi.


MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Steven Wasira akisalimiana na Mbunge wa Jimbo la Bariadi, Mhandisi Kundo Mathew mara baada ya kuwasili kwenye Mkutano wa hadhara Jimbo la Bariadi, uliofanyika katika Kijiji cha Ngulyati wilayani Bariadi.




















Je, una Tangazo, Picha za Matukio, Taarifa au Habari ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi 0746057557 au 0765402289 au Email : simiyupresstz@gmail.com

0 Comments

Post a Comment

Post a Comment (0)

Previous Post Next Post