Wachimbaji wa madini watakiwa kuzingatia usalama migodini.

Kamishna wa Tume ya Madini, Mhandisi Theonestina Mwasha akizungumza na wachimbaji wadogo wa mikoa ya Simiyu na Mara katika mafunzo ya usalama kwa wachimbaji wadogo wa madini na wadau wa sekta ya madini wa mikoa hiyo. (Picha na Derick Milton)

 

Wachimbaji wadogo wa Mkoa wa Simiyu na Mara katika mafunzo ya usalama kwa wachimbaji wadogo wa madini na wadau wa sekta ya madini wa mikoa hiyo. (Picha na Derick Milton)




Na Derick Milton, Bariadi.

 

Tume ya Madini imewataka wachimbaji wadogo wa madini kuhakikisha wanazingatia sheria, kanuni na miongozo ya usalama inayotolewa na wataalam wa sekta hiyo ili kukomesha ajali zinazoendelea kuripotiwa katika maeneo ya uchimbaji.

 

Wito huo umetolewa leo na Kamishna wa Tume ya Madini, Mhandisi Theonestina Mwasha, wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya usalama kwa wachimbaji wadogo wa madini na wadau wa sekta ya madini kutoka mikoa ya Simiyu na Mara yaliyofanyika mjini Bariadi, mkoani Simiyu.

 

Mhandisi Mwasha amesema Serikali kupitia Wizara ya Madini imejipanga kuwawezesha wachimbaji wadogo kwa kuwapatia elimu, vifaa na teknolojia ili kuwawezesha kujiinua kutoka katika uchimbaji wa kiwango cha chini hadi kuwa wachimbaji wa kati na baadaye wakubwa.

 

“Lengo kuu la mafunzo haya ni kuwaongezea uwezo wa kitaalam ili waweze kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazoikumba sekta hii, hususan katika maeneo ya usalama migodini,” amesema Kamishna Mwasha.

 

Aidha, amewataka wachimbaji hao kuzingatia matumizi salama ya kemikali, hususan zebaki, kwa kuwa matumizi mabaya yake yamesababisha madhara yasiyorekebishika kwa afya ya binadamu na mazingira.

 

“Mafunzo haya yamejikita katika sheria na kanuni za usalama mahali pa kazi pamoja na Sheria ya Madini. Ni muhimu sana kuhakikisha mnafuata miongozo hii katika kutekeleza shughuli zenu,” amesisitiza.

 

Kwa upande wake, Mkaguzi Mkuu wa Migodi kutoka Tume ya Madini, Mhandisi Hamis Kamando, amesema ajali nyingi zinazotokea migodini husababishwa na kutokuzingatia sheria na taratibu zilizowekwa na mamlaka husika.

 

Amebainisha kuwa baadhi ya ajali hizo zimesababisha vifo na ulemavu kwa wachimbaji, ambapo changamoto kubwa ni kuanguka kwa miamba, kuteleza katika ngazi na ukosefu wa hewa safi ndani ya maeneo ya uchimbaji.

 

“Ni wajibu wa kila msimamizi wa mgodi kuhakikisha hatua zote za kiusalama zinafuatwa kikamilifu ili kuzuia madhara haya,” ameongeza Mhandisi Kamando.

 

Naye Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Wadogo Mkoa wa Simiyu, Mashauri Ntizu, ameishukuru Tume ya Madini kwa kuandaa mafunzo hayo na kuyafikisha kwa wachimbaji wa mkoa huo.

 

“Mafunzo haya ni suluhisho la muda mrefu kwa changamoto zinazowakabili wachimbaji. Kupitia semina hii tumejifunza sheria, kanuni na mbinu bora za kufanya kazi kwa usalama,” amesema Ntizu.

 

Mafunzo hayo yanatarajiwa kuwafikia wachimbaji wadogo katika mikoa mingine nchini, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuboresha mazingira ya uchimbaji na kuimarisha mchango wa sekta ya madini katika pato la taifa.

 

Je, una Tangazo, Picha za Matukio, Taarifa au Habari ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi 0746057557 au 0765402289 au Email : simiyupresstz@gmail.com

0 تعليقات

إرسال تعليق

Post a Comment (0)

أحدث أقدم