Na Samwel Mwanga,Maswa.
MKUU wa mkoa wa Simiyu, Dkt Yahaya Nawanda ameridhishwa na hatua ya ujenzi wa shule mbili mpya za sekondari katika Kata ya Dakama na Kata ya Kulimi sambamba na ujenzi wa shule mpya ya Msingi katika kijiji cha Jija katika wilaya ya Maswa mkoa wa Simiyu.
Dkt Nawanda amesema hayo mara baada ya kufanya ziara ya siku moja katika wilaya hiyo na kukagua miradi mbalimbali inayotekelezwa katika wilaya ya Maswa.
Amesema kuwa watumishi wa Umma na wote wenye dhamana ya kusimamia miradi hiyo kuwa waadilifu na kuhakikisha miradi hiyo inakamilika kwa wakati uliopangwa na kwa ubora na viwango vinavyotakiwa.
Amesema kuwa serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan imetoa fedha nyingi kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika sekta elimu katika mkoa huo na ndiyo maana miradi ya ujenzi wa shule hizo unaendelea katika maeneo mbalimbali ndani ya mkoa wa Simiyu.
“Kwa sasa hivi tunafuatilia ujenzi huu wa shule mpya na madarasa wa fedha zilizotolewa na Rais Dkt Samia ili kuhakikisha kuwa Ujenzi huo unakamilika ndani ya muda uliopangwa na kwa ubora unaotakiwa,” amesema na kuongeza.
“Maelekezo ya Rais ni kukamilisha shule hizi na madarasa ifikapo mwanzoni mwa mwezi Desemba mwaka huu ili kuanzia mwezi Januari mwakani wanafunzi waanze kufundishwa katika shule hizo,”.
Akikagua ujenzi wa shule mpya za sekondari katika Kata ya Kulimi, Kata ya Dakama na Shule mpya ya Msingi katika kijiji cha Jija amesema kuwa serikali imeamua kufanya maboresho katika sekta ya elimu kwa kuboresha miundombinu ya shule kwa ajili ya kujifunza na kufundishia ili wanafunzi waweze kupata elimu bora.
Pia ameupongeza uongozi wa serikali wa wilaya pamoja na halmashauri ya wilaya hiyo kwa kuweza kusimamia ujenzi wa miradi hiyo ambapo amehaidi kutafuta kiongozi mkubwa wa kitaifa kwa ajili ya kuja kuifungua shule mpya ya msingi yenye mikondo miwili miwili katika kijiji cha Jija ambayo imejengwa kwa ubora unaotakiwa.
Pia amewataka Wazazi kuwapeleka shule watoto wao ili waweze kupata elimu kwa kuwa serikali kwa sasa inatoa elimu bila malipo kuanzia elimu ya Awali hadi kidato cha sita huku akitoa onyo kali kwa watu ambao wanajihusisha na mapenzi kwa wanafunzi wa kike na watakaobainika watachukuliwa hatua kali za kisheria.
Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Maswa, Maisha Mtipa akitoa taarifa za ujenzi wa shule hizo amesema kuwa wilaya hiyo ilipokea kiasi cha fedha zaidi ya Shilingi Bil.1 kwa ajili ya ujenzi wa shule mbili mpya za sekondari katika Kata ya Kulimi na Kata ya Dakama.
“Tulipokea fedha zaidi ya Shilingi Bilioni moja kwa ajili ya ujenzi mpya wa shule mbili mpya za sekondari katika wilaya yetu na sisi tukaona ni kata zipi ambazo hazina sekondari na tukabainisha kuwa ni Kata ya Dakama na Kata ya Kulimi hivyo kwa kila shule tumepatia kiasi cha Shilingi 548,280,029/-,”
“Pia tumepata zaidi ya shilingi Bilioni 1.5 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya BOOST kwa ajili ya kuboresha elimu ya Awali na Msingi na shule hii tuliyojenga katika kijiji cha Jija ambayo ina mikondo miwili miwili ya madarasa ni moja ya shule tuliyojenga kupitia mradi huo na imegharimu kiasi cha Shilingi 540,300,000/-,ámesema.
Naye Mkuu wa wilaya ya Maswa, Aswege Kaminyoge ametumia fursa hiyo kumshukuru Rais Dkt samia Suluhu kwa kuendelea kuwapatia fedha nyingi kwa ajilki ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika wilaya hiyo ikiwemo miradi ya elimu na kuhahidi kuzisimamia vizuri fedha zote zinazoletwa kwenye wilaya hiyo ili ziweze kufanya kazi kama zilivyokusudiwa.
“Nitumie fursa hii kumshukuru Rais Dkt Samia Suluhu kwa kuendelea kutuletea fedha nyingi sana katika wilaya yetu ya Maswa kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo hii miradi yah ii katika sekta ya elimu mie nahaidi kuendelea kusimamia fedha hizi ili ziweze kufanya kazi iliyokusudiwa,”amesema.
Miradi mingine iliyototembelewa na Mkuu huyo wa mkoa ni pamoja na Ujenzi wa Jengo la Utawala Halmashauri ya wilaya ya Maswa,Nyumba ya mtumishi katika shule ya sekondari ya Nyongo,Ukarabati wa shule ya Msingi Malampaka na Ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa na matundu ya vyoo matatu katika shule ya msingi Igunya.
MWISHO.
Je, una Tangazo, Picha za Matukio, Taarifa au Habari ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi 0746057557 au 0765402289 au Email : simiyupresstz@gmail.com
إرسال تعليق